Kiama cha wezi EPA chawadia
Rais wa Tanzania Jakaya Kikwete anatarajiwa kutangaza kiama cha wezi waliovuja pesa katika Akaunti ya Malipo ya Nje-EPA, baada ya kazi ya tume teule ya kuchunguza kashfa hiyo kufikia kikomo.Tume hiyo iliyokuwa ikiongozwa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Tanzania, Johnson Mwanyika, Mkuu wa Jeshi la Polisi Said Mwema na Mkurugenzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Edward Hosea, tayari imemaliza kazi hiyo na kupeleka majalada kwa mamlaka husika kwa hatua zaidi. Inaarifiwa kuwa Rais Kikwete ameamua kulishughulikia suala hilo kwa uhakika ili kurejesha imani ya serikali yake ambayo imekuwa ikipakwa matope kutokana na kashfa hiyo. Watakaokumbwa na rungu hilo ni wale walioshindwa kurejesha pesa walizoiba ambayo ni zaidi ya shilingi bilioni 133 ya Tanzania, lakini pia hata wale waliofanikisha uchotaji wa fedha hizo, nao wataguswa.